Makao Makuu - Dodoma
#CCM Imetimia KaziIendelee

Habari na Matukio Mbalimbali


RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI, AL HAJJ DK. HUSSEIN ALI MWINYI, AMEENDELEA KUIHIMIZA JAMII JUU YA UMUHIMU WA KUDUMISHA AMANI

alternative

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameendelea kuihimiza jamii juu ya umuhimu wa kudumisha amani na kubeba  imani ya dhati ndani ya mioyo yao kwa mustakbali wa taifa na ustawi wa jamii bora kwa maendeleo ya uchumi endelevu nchini.

Al hajj Dk. Mwinyi, alitoa nasaha hizo kwenye Msikiti Mabuluu Mfereji wa Wima, Mkoa wa Mjini Magharibi, alikojumuika pamoja na waumini wa dini ya Kiislamu kwenye ibada ya sala ya Ijumaa.

Rais, Al hajj Mwinyi, aliieleza Imani na amani ni vitu viwili vinavyokwenda sambamba na kutegemeana wakati wote, hivyo aliisihi jamii kadri wanapokusanyika pamoja kwenye maisha yao ya kila siku, wasichoke kuamini na kuendelea kuhimiza amani ya nchi na kuidumisha muda wote katika kuyaendea mazuri yote kwa ustawi wa jamii njema na taifa kwa ujumla.

“Imani na amani vinakwenda sambamba, amani ndio dini yetu, Uislamu unatutaka tueneze amani wakati wote, amani ikikosekana mambo mengine yote hayawezekani na hili tunalijua kutokana na wenzetu wanayoyapitia huko kwenye mataifa ya wenzetu, tunaona sehemu zenye vita hata ibada hazifanyiki, ili ipatikane amani lazima tuwe na Imani ndani ya nyoyo zetu” alisisitiza Al hajj Mwinyi.

Al hajj Dk Mwinyi alieleza, kila mmoja anawajibu wa kuitunza na kueneza amani kwa mustakbali wa taifa na ustawi wa jamii iliyobora.

Pia, aliwahimiza waumini hao kuendelea kuliombea taifa na viongozi kwa ujumla ili kuendelea kuwaongoza vyema na kuyatekeleza yote waliyowaahidi wananchi.

Rais Al Hajj Mwinyi alieleza, viongozi wanamajukumu makubwa na kubeba dhima kubwa hivyo, aliwasihi wanaumini hao na jamii kwa ujumla wasichoke kuwaombea mazuri na kuzidi kuwaombea kheir kwa Mwenyezi Mungu (S. W).

Akitoa nasaha za Ijumaa, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Sheikh Khalid Ali Mfaume, alisifu juhudi za Rais Al Hajj Dk. Mwinyi kwa Imani aliyoijenga kwa waumini wa dini ya kiislamu na taifa kwa ujumla ikiwemo kujumuika nao pamoja kwenye ibada katika misikiti mbalimbali nchini sambamba na kuwaboresha ustawi wa maendeleo na uchumi wananchi wote.

Alisema juhudi zote hizo ni Imani yake kwa Wazanzibari na taifa lote, hasa jitihada za kuendelea kuimarisha huduma za jamii, uchumi na maendeleo ikiwemo ujenzi wa miundombinu imara na kuboresha mawasiliano.

Naye, Khatibu wa sala ya Ijumaa msikitini hapo, Sheikh Abdul Karim Said Abdulla aliihusia jamii kuendelea kupendana na kutendeana mema kwa kujizuia kuudhiana na kutendea mabaya.

Aliwashajihisha waumini hao kuendeleza mshikamo kwa kudumisha amani, umoja na upendo baina yao kwa ustawi wa jamii iliyo njema.

alternative alternative alternative
Habari Nyingine

Nukuu za Viongozi