Makao Makuu - Dodoma
#CCM Imetimia KaziIendelee

Habari na Matukio Mbalimbali


MJUMBE WA KAMATI KUU YA HALMASHAURI KUU YA CCM TAIFA NDUGU HEMED SULEIMAN ABDULLA AMESEMA CHAMA CHA MAPINDUZI KITAENDELEA KUTEKELEZA ILANI YA CCM KWA KUIJENGA  ZANZIBAR YA KIUCHUMI

alternative

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Ndugu Hemed Suleiman Abdulla amesema Chama cha Mapinduzi kitaendelea kutekeleza Ilani ya CCM kwa kuijenga  Zanzibar ya kiuchumi kwa kutatua na kutekeleza ahadi zake kivitendo. Akizungumza na wana CCM na wananchi wa Jimbo la Magomeni na Jimbo la Kikwajuni amesema Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kushinda na kushikilia Dola kwa Vile Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi ana dhamira na nia thabiti ya kuwaletea Wazanzibari maendeleo endelevu. 

Mhe. Hemed ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kuwa nguzo pekee ya kukijenga na kukiimarisha Chama Cha Mapinduzi ni umoja na mshikamano ndani ya chama kwa viongozi kushirikiana katika kuwatumikia wanachama na wananchi wote kwa haki na usawa, ukweli na uwazi katika kukijenga Chama.

Amesema kumekuwa na makundi ya wapambe katika Chama yanayobeba Viongozi na wagombea ambapo ni vyema kuungana na kuacha kujenga mgawanyiko katika CCM na watumie ujuzi na nguvu zao katika kuunganisha wanachama kukiendeleza Chama Cha Mapinduzi. Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, amewataka Viongozi wa ngazi mbali mabali katika chama kujitahidi katika kusajili wanachama wapya, kusimamia wanachama waweze kulipa ada kwa wakati na kupatiwa kadi za kieletroniki.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Mjini Ndugu Talib Ali ameeleza kuwa kumekuwa na viongozi wa vyama vya upinzani wanapotosha umma wa wazanzibari kwa kuichafua Serikali ya Dkt. Mwinyi na kuwasihi wanachama wa Chama Cha Mapinduzi kueleza mazuri yanayofanywa na Viongozi wetu wanaopenda maendeleo. Amesema ikiwa wanachama wa CCM na wazanzibari wataungana pamoja hatutokuwa na mwanya kwa wasopenda maendeleo kuisema vibaya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Mjini Mhe. Rashid Simai Msaraka ameeleza kuwa Ziara ya hiyo ya Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ni ya mafanikio ambapo inadhihirisha utayari wa viongozi wakuu wa Serikali katika kukiimarisha Chama Cha Mapinduzi.

Mhe. Msaraka ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa Wilaya ya Mjini ameeleza kuwa kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020-2025 tayari utekelezaji wa Ilani hiyo umekamilika kwa asilimia Mia Moja (100) kwa kuzingatia sekta mbali mbali ikiwemo Michezo, Elimu, maji na miundombinu ya Barabara.

Kwa upande Viongozi wa Majimbo hayo wamemshukuru na kumpongeza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kutembelea Majimboni na kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM kwani ujio huo unatilia mkazo na kuwakumbusha majukumu yao. Wamemuhakikishia kuwa ushindi kwa Chama Cha Mapinduzi ni wa lazima katika majimbo hayo kwani wanachama wa CCM wameridhika na utekelezaji wa Ilani ya Chama kwa maendeleo yanayoletwa na Serikali ya Awamu ya nane inayoongozwa na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi .

Katika ziara hiyo Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ameweka Jiwe la Msingi ujenzi wa Tawi la CCM Nyerere 'A' pamoja na kukabidhi hati ya Nyumba iliyonunuliwa kwa ajili ya ujenzi wa Tawi la CCM Meya Bondeni ambapo ameupongeza Uongozi wa Jimbo la Magomeni kwa kuona umuhimu wa kuwa na majengo ya kisasa na ya kutosha kwa ajili ya watendaji wa Chama Cha Mapinduzi. Amesema ujenzi wa Ofisi hizo unadhihirisha juhudi za Viongozi wa Jimbo hilo kuunga mkono maelekezo ya Viongozi wakuu wa Chama Cha Mapinduzi kuwawekea mazingira mazuri watendaji ili wafanye kazi katika mazingira mazuri.

Aidha Mhe. Hemed ametembelea mradi wa maji Kikwajuni Mzimni ambao umesita kwa muda mrefu na kueleza kuwa Serikali itatafuta wataalamu kuangalia namna bora ya kukamilisha mradi huo ili uwafae wananchi wa maeneo hayo.

 

 

alternative alternative alternative
Habari Nyingine

Nukuu za Viongozi