Makao Makuu - Dodoma
#CCM Imetimia KaziIendelee

Habari na Matukio Mbalimbali


RAIS DK. HUSSEIN ALI MWINYI AIPONGEZA BENKI YA DUNIA KWA KUENDELEA KUIUNGA MKONO TANZANIA KUPITIA MIRADI MBALIMBALI YA MAENDELEO.

alternative

Rais Dk. Mwinyi ametoa pongezi hizo, Ikulu Zanznibar alipozungumza na Rais wa Benki hiyo, Ajay Singh Banga na ujumbe wake, wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano wa 20 wa Mapitio ya benki hiyo, unaotarajiwa kufanyika, ukumbi wa Golden Tulip, Uwanja wa ndege, Zanzibar.

Dk. Mwinyi alimueleza mgeni wake huyo juu ya Zanzibar inavyonufaika na fursa nyingi kutoka Benki ya Dunia, kupitia miradi ya kimkakati ya maendeleo ikiwemo miradi ya maji safi na utunzaji wa mazingira, umeme vijijini ambayo inatekelezwa Tanzania Bara.
Pia, Rais Dk. Mwinyi alieleza Zanzibar inavyonufaika na miradi ya huduma za jamii unayoungwa mkono na Benki ya dunia ikiwemo miradi ya uzalishaji umeme, maji safi na salama, miundombinu, uwezeshaji wa Wanawake, afya, elimu na Uchumi wa Buluu ambayo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Alisema, Zanzibar imekua na miradi mingi ya maendeleo inayoungwa mkono na Benki ya Dunia kupitia ushirikiano mzuri uliopo baina ya benki hiyo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Rais Dk. Mwinyi alieleza fursa nyengine ambapo Zanzibar inanufaika kutoka Benki ya dunia ni pamoja na kuwajengea uwezo Wanzania kupitia mikutano ya kimataifa, warsha, makongamano pamoja na misaada ya kiufundi. Mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu, Rais Dk. Mwinyi alitembelewa na Mwakilishi Mkazi wa Benki hiyo, Nathan Balete anaeziwakilisha nchi nyengine tatu za Afrika mbali na Tanzania zikiwemo Malawi, Zambia na Zimbawe.

Naye, Bw. Ajei Banga, alisifu juhudi za Rais Dk. Mwinyi kwa kuimarisha maendeleo na kuboresha huduma bora za jamii kwa wananchi wake na kueleza ushirikiano mzuri uliopo baina ya Tanzania na benki hiyo ikiwemo Zanzibar. Pia alisifu uzuri wa kisiwa cha Zanzibar na ukarimu wa watu wake waliojikita kwenye kuendeleza maendeleo. Kwa mara ya kwanza, Zanzibar inakua mwenyeji wa Mkutano mkubwa duniani wa Benki ya Dunia utakaohudhuriwa na wageni mashuhuri akiwemo rais wa Benki hiyo, Ajei Banga,
mkutano huo pia unaotarajiwa kuhudhuriwa kati ya wageni 300 hadi 350 wenye lengo la kufanya mapitio ya miradi inayoungwa mkono na benki hiyo, pamoja na mambo mengine pia utaangalia namna bora ya utekelezwaji wa miradi ya maendeleo na namna ya kuongezwa fedha na ruzuku kwa miradi itakayofanya vizuri zaidi kwa mataifa wanufaika.

Zanzibar pia inanufaika fursa za Benki ya Dunia kupitia sekta ya nishati hususani umeme wa jua, upepo na gesi asilia. Wakati huo huo, Rais Dk. Mwinyi amekutana na Balozi wa Qatar nchini Tanzania, Mhe. Fahad Rashid Al Marekhi aliyefika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo. Katika mazungumzo yao waligusia uhusiano uliopo kati ya Zanzibar na Qatar pamoja na fursa mbalimbali zilizopo Zanzibar ikiwemo uwekezaji, biashara, utalii, Uchumi wa Buluu, uvuvi, mafuta na gesi pamoja na huduma za kijamii hususani elimu na afya.

Rais Dk. Mwinyi alisema, licha ya sekta hizo kuwepo kwa kiwango kikubwa nchini lakini zinahitaji kuimarishwa zaidi ili kuwaondoshea wananchi changamoto zinazozikabili sekta hizo, hivyo aliomba ushirikiano zaidi ili kuimarisha sekta za maendeleo nchini pamoja na kulisifu ushirikiano mzuri uliopo baina ya Qatar na Tanzania ikiwemo Zanzibar.

alternative alternative alternative
Habari Nyingine

Nukuu za Viongozi