Makao Makuu - Dodoma
#CCM Imetimia KaziIendelee

Habari na Matukio Mbalimbali


ALICHOSEMA KATIBU MKUU WA CCM SAKATA LA CHADEMA KUSHIKILIWA POLISI

alternative

“Nimesikia kule Mbeya kulikuwa na tafrani kidogo kati ya Chadema na Polisi, na sisi kwa staili ya Rais wetu Samia Suluhu Hassan, anapenda sana mambo yawe yanamalizwa kwa kuzungumzwa, badala ya kukimbizana kimbizana kila mahali.

“Kwa hiyo nilifanya jitihada za kuwatafuta viongozi wenzangu wa vyama vingine ili nizungumze nao makatibu wenzangu, lakini nikaambiwa yule mmoja wa Chadema ni katika waliokamatwa. 

“Sasa nikasema kwa kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani uko hapa, mambo ya sheria, siyo ya kutolea maelekezo Kiongozi wa Chama cha siasa, au siyo? Lakini nitumie nafasi hii, mwambie Waziri wako, kwamba tunaomba, muone uwezekano wale viongozi wa vyama vya siasa waachiliwe. 

“Ili mtupate nafasi ya kuzungumza nao. Waachiliwe tupate nafasi ya kuzungumza nao, kwa sababu tunajenga taifa moja. Tunapenda kuwa na taifa tulivu.

“Kama kuna mahali wamekosea wao au tumekosea sisi, tukae tuzungumze. Tuijenge nchi yetu. Kwa hiyo huu ni ujumbe, mwambie Waziri wako kwamba Chama Cha Mapinduzi kinaamini kwamba kuzungumza ni jambo zuri zaidi. 

“Kabla vyombo vya sheria havijafanya mambo ya sheria basi mtupe nafasi kidogo sisi wanasiasa kwanza tuzumgumze," Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Katibu Mkuu wa CCM.

Balozi Nchimbi amezungumza hayo leo Agosti 12, 2024, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa CCM Katoro, mkoani Geita akiwa kwenye mwendelezo wa ziara yake ya siku 3, mkoani humo, aliyoanza Agosti 11, 2024.

Katibu Mkuu wa CCM huyo, katika ziara yake hiyo aliyoanzia Mkoa wa Kigoma, kisha Kagera na sasa yuko mkoani Geita, ameambatana na Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Ndugu Issa Haji Usi Gavu, Katibu wa NEC - Oganaizesheni, Ndugu Amos Gabriel Makalla, Katibu wa NEC - Itikadi, Uenezi na Mafunzo na Ndugu Rabia Hamid Abdalla, Katibu wa NEC - Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, ambapo kesho anatarajiwa kuzungumza na wananchi Mjini Geita, kwenye mkutano mkubwa wa hadhara utakaofanyika katika Uwanja wa Nyankumbu.

alternative
Habari Nyingine

Nukuu za Viongozi